1 Paulo na Barnaba walipofika katika mji Ikonio, wakaingia vilevile katika nyumba ya kuabudia ya Wayuda. Mule wakahubiri hata kundi kubwa la Wayuda na Wagriki wakaamini. 2 Lakini Wayuda waliokataa kuamini walishawishi watu wa mataifa mengine na kuwasukuma kuwachukia wandugu waamini. 3 Paulo na Barnaba wakakaa Ikonio kwa muda murefu. Walisema kwa uhodari kabisa, wakimutumainia Bwana. Naye aliwapa uwezo wa kufanya maajabu na vitambulisho. Na kwa njia hiyo alihakikisha kwamba ujumbe walioutangaza juu ya neema yake ulikuwa wa kweli. 4 Watu wa mji wakatengana: wamoja walikuwa upande wa Wayuda na wengine upande wa mitume. 7 5 Kisha Wayuda wamoja na watu wa mataifa mengine pamoja na wakubwa wao, wakakusudia kuwatendea mitume vibaya na kuwaua kwa kuwatupia mawe. 6 Paulo na Barnaba walipotambua jambo lile wakakimbilia katika mji wa Listra na wa Derbe ndani ya wilaya ya Likaonia na katika sehemu za kandokando yake. Kule wakaendelea kuhubiri Habari Njema. 8 Kule Listra kulikuwa mtu mmoja aliyekuwa kiwete tangia kuzaliwa. Yeye hakuweza kusimama wala kupima kutembea. 9 Yeye alikuwa akisikiliza mahubiri ya Paulo. Paulo akamukazia macho, naye akaona kwamba kiwete yule yuko na imani ya kuweza kuponyeshwa. 10 Halafu akamwambia kwa sauti: «Simama wima! Mtu yule akaruka akasimama na kuanza kutembea. 11 Wakati makundi ya watu walipoona jambo lile Paulo alilofanya, wakasema kwa sauti katika luga yao ya kilikaonia: “Miungu imetushukia ikiwa na sura ya kimtu!”» 12 Walimupanga Barnaba jina la mungu Zeu, na Paulo jina la mungu Herme, kwa sababu yeye ndiye aliyetoa hotuba. 13 Naye kuhani wa hekalu la mungu Zeu, lililokuwa kwenye kiingilio cha mji, akaleta ngombe waliopambwa na mafungu za maua mbele ya mulango. 14 Lakini mitume Barnaba na Paulo waliposikia habari ile, wakapasua nguo zao kwa huzuni, wakaingia haraka katikati ya kundi la watu, na kusema kwa sauti: 15 «Wandugu, kwa sababu gani munafanya mambo kama haya? Sisi vilevile ni watu, tuko sawasawa nanyi, na tunawahubiri ninyi Habari Njema kwamba muache kuabudu vitu hivi vya bure na mumugeukie Mungu mwenye uzima; yeye aliyeumba mbingu na dunia, bahari na vyote vinavyokuwa ndani yao. 16 Katika siku zilizopita Mungu aliwaachilia watu wa mataifa yote wafuate njia wanazotaka. 17 Ingawa vile hakuacha kujijulisha kwa njia ya kutenda mema. Anawanyeshea mvua toka mbingu, anawapa mavuno kwa wakati wake, anashibisha mioyo yenu na chakula na kuwajaza na furaha.» 18 Ijapokuwa mitume walisema maneno haya, ilikuwa vigumu kuzuiza makundi ya watu wasiwatolee sadaka. 19 Kisha Wayuda wamoja wakakuja tokea katika mji wa Antiokia na wa Ikonio. Wakashawishi makundi ya watu wajiunge nao. Wakamutupia Paulo mawe na kumukokotea inje ya mji, wakizani kwamba amekwisha kufa. 20 Lakini wanafunzi walipokuwa wakimuzunguka, akasimama na kurudi ndani ya mji. Kesho yake yeye pamoja na Barnaba wakaenda katika mji wa Derbe. 21 Paulo na Barnaba walihubiri Habari Njema katika mji wa Derbe, na kupata wanafunzi wengi. Kisha wakarudi katika mji wa Listra, wa Ikonio na wa Antiokia ya Pisidia. 22 Kule waliwajenga wanafunzi moyo na kuwatia nguvu wabakie katika imani wakiwaambia: «Ni sherti tupite katika mateso mengi kwa kuweza kuingia katika Ufalme wa Mungu.» 23 Wakawachagua wazee katika kila kanisa. Na kisha kuomba na kufunga kula chakula, wakawaweka chini ya ulinzi wa Bwana waliyemwamini. 24 Kisha wakapitia katika jimbo la Pisidia na kufika katika inchi ya Pamfilia. 25 Walipokwisha kuhubiri Neno la Mungu kwa watu wa mji Perga, wakaenda katika mji wa Atalia. 26 Na kutoka kule wakarudi mpaka Antiokia kwa njia ya chombo. Ni kule walipokuwa wameombewa neema kwa Mungu kwa ajili ya kazi ile waliyotoka kutimiza. 27 Walipofika Antiokia, wakafanya mkutano wa kanisa na kuwaelezea mambo yote Mungu aliyofanya kwa njia yao, na namna alivyowafungulia watu wa mataifa mengine mulango kusudi wao vilevile wapate kuamini. 28 Nao wakakaa kule Antiokia kwa muda wa siku nyingi pamoja na wanafunzi.