1 Jambo la lazima sana katika maneno tunayosema sasa ni hili. Tuko na Mkubwa wa namna ile, anayeikaa na mamlaka katika mbingu kwa kuume kwa Mwenyezi Mungu. 2 Yeye anafanya kazi ya Kuhani Mkubwa katika Pahali Patakatifu Sana, maana yake katika hema ya kweli iliyosimikwa na Bwana, wala si mtu. 3 Kila Kuhani Mkubwa anawekwa kusudi afanye kazi ya kutoa sadaka na matoleo. Kufuatana na hiyo, ilimupasa Kuhani wetu Mkubwa Kristo akuwe na kitu cha kutoa vilevile. 4 Kama Kristo angekuwa katika dunia, asingekuwa kuhani hata kidogo, kwa sababu kuko makuhani wanaotoa sadaka kufuatana na maagizo ya Sheria. 5 Kazi wale makuhani wanayofanya ni mufano na kitambulisho kinachoonyesha jinsi mambo kamili yanavyopitika mbinguni. Maneno hayo yanalingana na yale yaliyomutokea Musa. Wakati Musa alipokuwa karibu ya kujenga Hema, Mungu alimwambia: «Ufanye angalisho kusudi upate kutengeneza kila kitu kufuatana na mufano niliokuonyesha kwa mulima.» 6 Lakini sasa Yesu amepewa kazi inayokuwa bora zaidi kuliko kazi ya wale makuhani, kwa maana yeye ni mupatanishi wa agano linalokuwa zuri zaidi. Sherti za agano lile zinasimamia juu ya ahadi ya Mungu inayokuwa bora zaidi. 7 Kama lile agano la kwanza lingekuwa kamilifu, haingekuwa lazima likombolewe na la pili. 8 Lakini Mungu aliwaonya watu wake, akisema: «Katika siku zinazokuja, nitafanya agano jipya na watu wa ufalme wa Israeli na wa Yuda. Ni Bwana anayesema hivyo. 9 Agano lile halitakuwa sawa na lile nililofanya na babu zao siku nilipowakamatia kwenye mukono na kuwaondoa toka inchi ya Misri. Kwa sababu hawakushika lile agano, kwa hiyo vilevile sikuwashugulikia. Ni Bwana wetu Mungu anayesema hivyo. 10 Sasa hili ndilo agano nitakalofanya na watu wa ufalme wa Israeli katika siku zile: nitawawezesha kuchunga sheria zangu ndani ya mafikiri yao, nikiziandika ndani ya mioyo yao. Ni Bwana wetu Mungu anayesema hivyo. Nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. 11 Hakutakuwa tena atakayefundisha mwanainchi mwenzake, au kumwambia ndugu yake: “Umujue Bwana. Kwa maana watu wote watanijua, tangu mudogo mpaka mkubwa. 12 Mimi nitawasamehe maovu yao, wala sitakumbuka tena zambi zao.”» 13 Mungu alipotangaza hilo agano kuwa jipya, jambo hilo lilisababisha lile la kwanza kuwa la zamani na lenye kuchakaa. Na kitu chochote kikiwa cha zamani na chenye kuchakaa kinafikia wakati wa kutoweka.