Sura 3

1 Kwa sababu hiyo, wandugu zangu, ninyi ambao mumeitwa na Mungu na kuwa watu wake kama vile sisi, mufikiri sana juu ya Yesu, anayekuwa mutume na Kuhani Mkubwa wa imani tunayotangaza. 2 Yeye alikuwa mwaminifu mbele ya Mungu aliyemusimika kwa kazi ile, sawa vile Musa alivyokuwa mtumishi mwaminifu katika kazi ya nyumba yote ya Mungu. 3 Mujengaji wa nyumba anaheshimiwa zaidi kuliko nyumba yenyewe. Hivi vilevile Yesu anastahili kupewa heshima kubwa zaidi kuliko Musa. 4 Ni kweli kila nyumba inajengwa na mtu, lakini Mungu ndiye aliyejenga vitu vyote. 5 Musa alikuwa mtumishi mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu, kusudi ashuhudie maneno ambayo Mungu angesema nyuma. 6 Lakini Kristo ni mwaminifu kama Mwana anayesimamia nyumba ya Mungu. Na sisi ndio nyumba ile, kama tukiendelea kuwa na uhodari na kuaminia kupata mambo tunayotumainia. Mapumziko Mungu anayotayarishia watu wake 7 Kwa hiyo, kama vile Roho Mtakatifu anavyosema: «Leo ikiwa munasikiliza sauti ya Mungu, 8 musifanye mioyo yenu kuwa migumu kama babu zenu walivyofanya wakati walipomuasi Mungu, sawa siku ile walipomupima katika jangwa. 9 Kule babu zenu walinipima na kunijaribia, ingawa walikuwa wameona yote niliyotenda kwa muda wa miaka makumi ine. 10 Kwa sababu ile nilikasirikia kizazi chao, na kusema: Watu hao wanapotoka mioyo siku zote. Nao hawafuati njia zangu. 11 Basi nikaapa kwa kasirani kwamba hawataingia kwenye mapumziko niliyowatayarishia!» 12 Basi wandugu zangu, muangalie vizuri, kati yenu kusikuwe mtu mmoja mwenye moyo mubaya wa kutokuamini, aliyefikia hata kujitenga mbali na Mungu Mwenye Uzima. 13 Lakini muonyane kila siku kwa muda wote ambao lile neno leo linalotajwa lingali linatuelekea kusudi hata mmoja wenu asikuwe mugumu kwa kudanganywa na zambi. 14 Kwa maana sisi wote tunaishi katika ushirika na Kristo ikiwa tunachunga mpaka mwisho lile tumaini tulilopata kwa mwanzo. 15 Maandiko Matakatifu yanasema: «Leo ikiwa munasikiliza sauti ya Mungu, musifanye mioyo yenu kuwa migumu kama babu zenu walivyofanya wakati walipomuasi Mungu.» 16 Ni watu gani waliosikia maneno ya Mungu na kumwasi? Si wale wote walioongozwa na Musa toka katika inchi ya Misri? 17 Tena, ni watu gani waliomukasirisha Mungu kwa muda wa miaka makumi ine? Si wale wote waliofanya zambi wakaanguka na kufa katika jangwa? 18 Tena ni watu gani Mungu aliowaapia kwamba hawataingia kwenye mapumziko aliyowatayarishia? Si wale waliokataa kumutii? 19 Basi tunaona kwamba hawakuweza kuingia kwenye mapumziko yale kwa sababu ya kutokuamini kwao.